A TOWN BOYS ARUSHA

SIMANZI KUBWA NCHINI

Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, akitoa heshima za mwisho kwa mwili wa Dk Sengondo Mvungi aliyefariki dunia Novemba 12, nchini Afrika Kusini, katika Viwanja vya Karimjee Dar es Salaam jana. Kulia ni Waziri Mkuu mstaafu

Kwa ufupi
Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal aliwaongoza viongozi mbalimbali wakiwemo Rais mstaafu, Benjamin Mkapa, mawaziri wakuu wastaafu, mawaziri, wabunge, viongozi wa vyama vya siasa na viongozi wa dini, kuuaga mwili wa Dk Mvungi kwenye Viwanja vya Karimjee, jijini Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Simanzi na vilio jana vilitawala wakati wa kuaga mwili wa aliyekuwa Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Dk Sengondo Mvungi aliyefariki dunia kwenye Hospitali ya Milpark nchini Afrika Kusini alikopelekwa kwa matibabu.
Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal aliwaongoza viongozi mbalimbali wakiwemo Rais mstaafu, Benjamin Mkapa, mawaziri wakuu wastaafu, mawaziri, wabunge, viongozi wa vyama vya siasa na viongozi wa dini, kuuaga mwili wa Dk Mvungi kwenye Viwanja vya Karimjee, jijini Dar es Salaam.
Watu wengi waliowasili katika viwanja hivyo saa 3:00 asubuhi walionekana wenye huzuni, huku wakikaa katika makundi wakizungumza kwa sauti za chinichini.
Ilipofika saa 4:00 asubuhi, mvua ilianza kunyesha na kuwalazimisha watu waliokuwa wametawanyika katika eneo hilo kuanza kutafuta sehemu ya kujificha.
Dakika tatu baadaye wakati mvua ikiendelea kunyesha, gari lililokuwa limebeba mwili wa Dk Mvungi liliwasili kwenye viwanja hivyo, kitendo kilichowafanya baadhi ya waombolezaji kuanza kutokwa machozi.
Mara baada ya mwili kuwekwa sehemu iliyokuwa imeandaliwa, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Paramagamba Kabudi alipanda jukwaani kusoma historia ya marehemu.
Kabudi alisema Dk Mvungi alikuwa mtu aliyechukia rushwa na kuheshimu utawala bora, na kwamba kifo chake kimewaunganisha pamoja watu wa itikadi tofauti.
Aliongeza kuwa kutokana na uzalendo aliokuwa nao kwa nchi yake, Dk Mvungi alipomaliza mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), baada ya kumaliza elimu ya sekondari, aliendelea kuvaa magwanda hayo alipokuwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam hadi yalipochakaa.
Aliongeza kuwa, Dk Mvungi ambaye pia alikuwa mwanasheria maarufu nchini, alishiriki kubadilisha mfumo wa masomo ya sheria vyuo vikuu baada ya kuanzisha utaratibu wa kusoma shahada ya sheria kwa miaka minne tofauti na mitatu ya awali.
“Mwaka 1998 aliitisha kikao mjini Arusha na kushawishi kubadili shahada ya sheria kutoka miaka mitatu ya awali hadi minne ya sasa,” alisema.
Akizungumzia uamuzi wa Dk Mvungi kugombea kiti cha urais mwaka 2005, Kabudi alisema kwamba Mvungi hakugombea kiti hicho kwa sababu alikuwa anajua angeshinda au alikuwa anamchukia rais aliyekuwa madarakani wakati huo, bali alitaka kushiriki ndiyo maana aliposhindwa alikuwa wa kwanza kukubali matokeo.
Akiongoza misa ya kuuaga mwili wa marehemu, Padri Monsinyori Deogratius Mbiku alisema kuwa Dk Mvungi ameshakamilisha kazi yake hapa duniani, hivyo ni wajibu wa kila mtu kuhakikisha anatekeleza majukumu aliyopewa.

Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment