A TOWN BOYS ARUSHA

JOSEPH KAPINGA; TUMECHOKA, SIKIO LA KUFA LISIKIE DAWA SASA

Ukiombwa utoe sababu kwa nini michezo nchini imeshindwa kuleta tija hasa katika eneo la kimataifa, bila shaka kapu kubwa litahitajika ili kujaza sababu hizo kutokana na ukweli kwamba ziko nyingi.
Japo nizitaje chache. Hakuna uwekezaji wenye dhamira ya dhati kuinua michezo kuanzia ngazi za chini, ambako ndiko kwenye kiini cha vijana wengi wenye vipaji.
Nchi pia haina wataalamu wenye uwezo kubaini vipaji vya vijana chipukizi na kuviendeleza. Makocha maalumu wa vipaji tuliona wanabahatisha kufanya kazi hiyo.
Kadhalika, sapoti ndogo ya Serikali kusaidia sekta ya michezo nayo ni miongoni mwa sababu. Sekta hii kila mwaka imekuwa ilalamika kutengewa fungu dogo lisilokwenda na mahitaji husika.
Lakini pia suala la wakuu na viongozi wetu kuingiza siasa kwenye mambo yanayohitaji utaalamu, ni tatizo kubwa lililokosa dawa ya kulitibu. Na hili ndilo tatizo la msingi kwa nini michezo inashindwa kusonga mbele. Viongozi wetu ni wale wale, hawana ubunifu wameendelea kuwa watumwa wa kuongoza kwa mazoea.
Inashangaza, kwa sababu hata kama atakuja kiongozi mpya nje ya wale wa kila siku, atakachokifanya ni kile kile. Mfumo wetu wa uongozi umeshaharibika. Mfano mdogo. Klabu za Simba na Yanga ndizo zinazoongoza kwa madeni ya kujitakia na baadhi yake yamezifikisha timu hizo mahakamani, jambo ambalo ni aibu kubwa.
Klabu hizi zina utumwa wa kuwatimua makocha na wachezaji bila kufuata taratibu na matokeo yake kujikuta zililazimika kulipa fedha nyingi kama fidia. Tatizo ni kuongoza kwa mazoea, alichokifanya kiongozi aliyetangulia hakiwi fundisho kwa kiongozi anayefuata. Atafanya vile vile ilivyokuwa kwa mtangulizi wake. Nitakuwa sahihi kusema michezo nchini haina nafasi ya kupiga hatua. Tukiendelea kulea utamaduni wa kuwachagua viongozi kwa kufuata matakwa binafsi na siyo mahitaji ya kukuza michezo, tusishangae kuona tunapiga hatua mbili mbele, moja nyuma.
Kinachoshangaza ni kwamba, kuna mifano mingi ya kimageuzi katika sekta ya michezo kimataifa, lakini viongozi wetu wameshindwa kujifunza. Walichong’ang’ania ni siasa za majungu na fitina.
Ipo sababu wadau wa soka waseme sasa basi, tunahitaji viongozi wabunifu watakaokuja na taswira mpya ya uongozi. Sishawishiki kuamini kwamba hatuna viongozi wa aina hiyo, tunao wengi katika kila mchezo.
Tatizo kubwa lililopo ni mifumo yetu ya uongozi. Kila sehemu wamejipanga walewale, wanapokezana madaraka kama Simba na Yanga zinavyopokezana kutwaa ubingwa Bara. Tusitosheke na dhana kwamba; ‘sikio la kufa halisikii dawa’.

Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment