A TOWN BOYS ARUSHA

Uhamiaji yatoa ufafanuzi ajira zilizositishwa

Dar es Salaam. Wizara ya Mambo ya Ndani imetoa ufafanuzi kuhusu ajira zilizositishwa na kusema siyo zile zilizoandikwa na vyombo mbalimbali vya habari jana.
Jana vyombo vya habari viliandika kuwa ajira 70 za Idara ya Uhamiaji kwa nafasi ya Mkaguzi Msaidizi Uhamiaji zilisitishwa baada ya kuwapo na madai ya upendeleo.
Msemaji wa Wizara hiyo, Isaac Nantanga, alisema taarifa zilizoandikwa kuhusu kusitishwa ajira 70 zilizopatikana baada ya usaili uliofanyika Uwanja wa Taifa hivi karibuni hazikuwa sahihi.
“Ukweli ni kuwa usaili wa nafasi ya Mkaguzi Msaidizi wa Uhamiaji ambao awali ulianzia Uwanja wa Taifa ulikwenda vizuri hadi wakapatikana wasailiwa wa kujaza nafasi 70 za Mkaguzi Msaidizi wa Uhamiaji. Usajili huo haukuwa na matatizo yoyote na waliochaguliwa walitakiwa kuripoti kazini  Julai 29, lakini kwa sababu ya sikukuu sasa wataripoti baada ya sikukuu,” alisema.
Alifafanua kuwa wasailiwa waliochaguliwa kujaza nafasi 70 za Mkaguzi Msaidizi wa Uhamiaji hawahusiki na usitishwaji uliotangazwa juzi na wanatakiwa kuendelea na mipango ya kuripoti kazini kama ilivyotangazwa hapo awali.
Wasailiwa wanaohusika na kusitishwa kwa ajira zao ni wale waliokuwa wameshiriki katika zoezi la kuajiri Konstebo na Koplo wa Uhamiaji ambao idadi yao ni 200 na kutakiwa kuripoti Agosti 6, lakini wameelekezwa kusubiri hadi watakapopewa maelekezo mengine.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Mbarak Abdulwakil amesitisha ajira za Konstebo na Koplo wa Uhamiaji zilizotangazwa na Idara ya Uhamiaji hivi karibuni.
Hatua hiyo imechukuliwa kutokana na tuhuma zilizotolewa na baadhi ya vyombo vya habari na mitandao ya kijamii kuwa kulikuwa na upendeleo kwa ndugu na jamaa za watumishi wa Idara hiyo.
Kutokana na hatua hiyo, Abdulwakil ameunda Kamati ndogo ya Uchunguzi itakayochunguza tuhuma hizo.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment