A TOWN BOYS ARUSHA

Zijue aina za mikataba ya ajira

Ule msemo wa kazi nzuri ukiwa hujaipata na huwa mbaya ukiwa nayo, unaweza ukaonyesha uhalisia wakati unapopaswa kufahamu ni aina ipi ya mkataba wa ajira uliosainiwa kati ya mwajiri na mwajiriwa.
Aina ya mkataba wa ajira huonyesha mustakabali wa ajira yenyewe, humpa mfanyakazi na mwajiri fursa ya kufahamu haki na wajibu wa kila upande na hivyo kujenga mazingira mazuri ya utekelezwaji wake kwa kulinda masilahi ya kila upande.
Mkataba wowote ule unaoingiwa kati ya pande mbili, ni lazima uwe na vigezo vikuu vya mkataba ikiwamo makubaliano ya pande mbili, malipo halali, lengo halali, uwezo wa kuingia mkataba na hiyari.
Bila kujali ni aina ipi ya mkataba wa ajira mliosaini, kama kimojawapo kati vigezo vikuu vya uhalali wa mkataba kitakosekana, kinaweza kuufanya mkataba wenyewe kuwa batili tangu mwanzo.
Kwa mujibu wa kifungu cha 14 cha sheria ya ajira na uhusiano kazini ya mwaka 2004, mikataba ya ajira iko ya aina tatu ambayo ni; mkataba usiokuwa na muda maalumu, mkataba wa muda maalumu kwa wataalamu na kada ya uongozi pamoja na mkataba wa kazi maalumu.
Mkataba usiokuwa na muda maalumu ni ule ambao unasainiwa kati ya mwajiri na mwajiriwa, ambao unaweza kuonyesha tarehe uliyosainiwa lakini hauonyeshi au hauelezi kuwa utaisha lini. Mikataba ya namna hii mara nyingi huwa katika taasisi za umma na baadhi ya taasisi binafsi.
Aina ya pili ya mkataba wa ajira ni mkataba wa muda maalumu kwa kada ya uongozi. Aina hii ya mkataba huhusisha zaidi kada ya uongozi au mwajiriwa mwenye fani ya aina fulani ambaye huajiriwa kushika wadhifa fulani wa juu katika utekelezaji wa majukumu yake. Hata hivyo aina nyingine za waajiriwa wanaweza pia kuwa na mkataba wa muda maalumu bila kujali kada anayotoka kulingana na mahitaji maalumu ya mwajiri.
Aina ya tatu ya mkataba wa ajira ni mkataba kwa kazi maalumu. Mkataba huu unaweza kupewa kipindi maalumu cha kumalizika au mara nyingi kumalizika kwake hutegemea kumalizika kwa kazi husika ambazo mwajiri na mwajiriwa watakuwa wamekubaliana kutekeleza.
Hii yaweza kuhusu utekelezaji wa mradi fulani au shughuli maalumu ambayo kuisha kwake ndiyo huashiria kufikia mwisho kwa mkataba wa ajira.
Jambo la muhimu na la kuzingatia ni kwamba kifungu cha 15 cha sheria ya ajira na uhusiano kazini, kinamtaka kila mwajiri na mwajiriwa kuhakikisha kuwa kabla ya kuanza kazi, kuna mkataba wa maandishi uliosainiwa kati ya pande hizo mbili.
Mkataba ndiyo utakaoeleza aina ya shughuli utakazofanya, mipaka, unawajibika kwa nani, malipo yako, haki zako za msingi, namna ya kuvunja mkataba na masuala mengine muhimu ambayo hamuwezi kukubaliana tu kwa maneno.
Tatizo kubwa la mkataba wa maneno ni ugumu wa kuuthibitisha. Kukosekana kwa mkataba wa maandishi kunahatarisha ulinzi na usalama wa haki na wajibu wa mwajiri na mwajiriwa. Usikubali kuanza kazi bila mkataba.Usikubali kusaini mkataba bila kuusoma na kuuelewa pia ni muhimu kujua umeingia mkataba wa aina gani kati hizo aina tatu nilizoeleza hapo juu, ili ujue haki na wajibu wako kisheria na namna gani maslahi yako kama mwajiri au mwajiriwa yanaweza yakalindwa pasipo vikwazo vya aina yoyote.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment